Mahakama ya juu zaidi nchini Kenya, imeamua kuwa rais mteule Uhuru
Kenyatta atasalia kuwa rais mpya wa Kenya baada ya kusema kuwa uchaguzi
ulifanywa kwa njia huru na ya haki.
Uchaguzi wenyewe ulifanyika tarehe nne mwezi Machi, ambapo hesabu ya
kura ilimpa ushindi Kenyatta kwa zaidi ya laki nane.
Rais wa mahakama hiyo jaji mkuu Willy Mutunga alisema kuwa mahakama
imekubali kwa kauli moja kuwa uchaguzi ulifanywa kwa njia ya huru na wazi na
kuwa Kenyatta na mgombea mwenza wake walichaguliwa kihalali.
Uamuzi huu una maana kuwa Uhuru Kenyatta ndiye ataapishwa kama rais
mpya wa Kenya tarehe tisa mwezi ujao
Kesi hiyo iliwasilishwa katika mahakama ya juu zaidi na mpinzani mkuu
wa Kenyatta, Raila Odinga baada ya uchaguzi uliofanyika mapema mwezi huu.
Matokeo rasmi yalionyesha kuwa Uhuru alishinda uchaguzi kwa kumpiku
Raila kwa asilimia 50.07 huku Raila akipata asilimia 43.28. Matokeo haya
yalizuia kufanyika kwa duuru ya pili ya uchaguzi kwa kura 8,100.
Bwana Odinga aliishutumu tume huru ya uchaguzi na mipaka kwa kuhujumu
matokeo ya uchaguzi ili kumpa ushindi Uhuru Kenyatta.








