Mahakama ya Juu (Supreme Court) nchini Kenya jana ilitupilia mbali viapo
viwili katika kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi yaliyompa ushindi Uhuru
Kenyatta wa Muungano wa Jubilee.
Maombi yaliyotupwa ni lile la muungano wa mashirika yasiyo ya
kiserikali lililoitaka mahakama iamuru tume ya uchaguzi kufikisha mahakamani
hapo nyaraka zote zilizotumika wakati wa uchaguzi huo.
Kadhalika mahakama hiyo ilitupilia mbali hati ya kiapo yenye kurasa 839
kilichowasilishwa na upande wa Muungano wa Cord ambacho kilidai kwamba kura
katika majimbo 120 zilikuwa haziwiani na idadi ya wapigakura, hivyo kuitaka
mahakama hiyo iitishe uchunguzi wa kina kwa daftari hilo pamoja na kura
zilizopigwa.







