Language

Tuesday 16 April 2013

MUHIMBILI KWISHA HABARI YAKE, NI WAGONJWA 7 TU WANAOWEZA KUHUDUMIWA



Kituo cha Afya ya Akili cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kilichopo Chamazi Mbagala kina uwezo wa kuhudumia wagonjwa saba tu imefahamika.

Hali hiyo imekuwa ikisababisha wagojwa wengi wenye tatizo hilo kushindwa kupata huduma au kupata katika hali isiyo na ubora.
Akijibu swali bungeni jana, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Agrey Mwanri, alisema awali kituo hicho kilikuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa 32.
Mwanari alisema kutokana na kituo hicho kuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa wachache, Hospitali ya Muhimbili haipeleki wagonjwa katika kituo hicho kama ilivyokuwa siku za nyuma.
Mwanri alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Mariam Kisangi (CCM), aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuendeleza kituo hicho ambacho ni muhimu kwa wagonjwa wa akili.

Naibu Waziri alisema, Hospitali ya Muhimbili inaendela na juhudi za kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati wa kituo hicho, ili kutoa huduma kwa wagonjwa wengi zaidi.
“Mpango wa baadaye kwa ajili ya kituo hicho ni pamoja na kukiendeleza ili kiweze kutoa huduma kwa wagonjwa walioathirika na dawa za kulevya, alisema Mwanri.
Alivitaja vituo vingine vinavyotoa huduma ya aina hiyo ni Kituo cha Hombolo Dodoma ambacho ni sehemu ya Hospitali ya Milembe na Lutindi kilichopo Korogwe ambacho kinamilikiwa na Shirika la dini.
Alisema Muhimbili imeanza utaratibu wa kupata mshauri mwelekezi ili kuishauri namna ya kuboresha matumizi ya ardhi katika kituo hicho.
Baadhi ya wabunge wanaishauri Serikali kuonyesha kujali wagonjwa wa akili kwa kufanya mkakati wa haraka wa kuhakikisha huduma zinapatikana.
Nchini kuna watu wengi wenye kusumbuliwa na tatizo hilo, mojawapo ya sababu ikielezwa kuwa msongo wa mawazo na staili za maisha, achilia mbali historia ya familia na magonjwa mengine.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...