Language

Thursday 28 February 2013

HABARI MUHIMU: MAGARI YA ZIMAMOTO YAMETAJWA KUVUSHA MALI ZA WIZI UWANJA WA NDEGE WA JK NYERERE DAR

IMEBAINIKA kuwapo kwa wizi wa kutisha katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, huku magari ya Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji yakitajwa kwamba yamekuwa yakivusha vifaa vya wizi kutoka ndani ya uwanja huo.

Wizi huo ambao umewasababishia hasara kubwa baadhi ya wasafiri wakiwamo wafanyabiashara, abiria wa kawaida na watalii wanaoingia nchini, unadaiwa kufanywa na baadhi ya wafanyakazi wa Wakala wa Mizigo wa Kampuni ya Swissport.
Wafanyakazi hao wamekuwa wakiiba vifaa na bidhaa kwa kuchana mabegi ya abiria kisha kuviweka kwenye makoti yao ya kazi lakini kwa mizigo mikubwa, wamekuwa wakiificha kwenye magari ya zimamoto ambayo huingia na kutoka ndani ya uwanja wa ndege bila kufanyiwa ukaguzi.
Chanzo kingine cha habari katika uwanja huo kinasema magari ya zimamoto yanayofanya kazi katika uwanja huo hayakaguliwi yanapopita kwenye lango kuu, hivyo kutoa mwanya wa kuvushwa kwa mali za wizi.
“Mali zinazowekwa katika magari hayo ni zile kubwa ambazo hutakiwa kuuzwa nje ya uwanja wa ndege kama kontena la simu au mabegi makubwa ya nguo,” kilisema chanzo hicho.
Baadhi ya waathirika wa wizi huo waliliambia gazeti hili kwamba wamepoteza mizigo mingi kwa nyakati tofauti na kupata hasara kubwa na kwamba uwanja huo si salama kwa wafanyabiashara hasa wanaoingiza bidhaa zao kutoka nje ya nchi.
Chanzo chetu katika uwanja huo kilidokeza kuwa mara nyingi wizi hufanyika wakati mizigo inaposhushwa kutoka kwenye ndege kupelekwa eneo la kusubiri kuchukuliwa na abiria pia wakati mizigo mingine inapohifadhiwa kwenye stoo uwanjani hapo ikisubiri wahusika kuichukua.
“Wakati wanashusha mizigo kutoka kwenye ndege wanaikata kwa visu au viwembe vikali na kuchomoa chochote kilichomo kisha wanaweka katika makoti ya kazi ambayo yana mifuko mikubwa,” kilieleza chanzo hicho.
Mkurugenzi Mtendaji wa Swissport Tanzania, Gaudence Temu alikiri kuwapo kwa tatizo hilo lakini akasema kampuni yake kwa kushirikiana na wadau wengine uwanjani hapo wamekuwa wakichukua hatua za kudhibiti wizi huo.
“Huu wizi unaharibu sifa ya uwanja wa ndege wa kimataifa, ndiyo maana tukasema hatutakuwa na uvumilivu hata kidogo kwa wale ambao tunabaini kwamba wanafanya vitendo hivyo,” alisema Temu.
Kamishna Msaidizi wa Zimamoto na Uokoaji, Sikiri Sala alisema amekwishazungumza na Kikosi cha Zimamoto Uwanja wa Ndege kuhusu suala hilo ambalo hata hivyo, alisema ni zito na linahitaji ushirikishwaji wa viongozi wote kwa kuwa uwanja huo una mashirika mengi.
“Wadau wengi wanapaswa kuzungumzia suala hili. Kuna polisi wa usalama uwanja wa ndege, kuna watu wa usalama, TAA (Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania) na kampuni za mizigo kama Swissport. Hawa wote wanatakiwa kufahamu suala hili kwa sababu lina uzito,” alisema Sala.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...