Language

Wednesday 17 April 2013

UHURU KENYATTA JINO KWA JINO NA WAENDEKEZA RUSHWA KENYA



Rais mpya wa Kenya, Uhuru Kenyatta amefungua rasmi Bunge la nchi yake kwa kutangaza vita dhidi ya rushwa ambayo imekithiri katika idara nyingi za Serikali.

Akizungumza kwa kujiamini kwenye Ukumbi wa Bunge uliokarabitiwa hivi karibuni, Kenyatta alieleza kwamba hivi sasa anaandaa safu ya mawaziri makini watakaomsaidia kuendesha Serikali yake na watakaohakikisha anatimiza agenda zake muhimu.
Katika hotuba yake kwa wabunge na maseneta jijini Nairobi, Kenyatta alisema kwamba suala la rushwa limekuwa kikwazo katika utoaji huduma.
Kenyatta pia alitaja vipaumbele vinane muhimu katika Serikali, ambavyo ni kuhakikisha kunakuwepo uwazi katika utoaji wa huduma za jamii, kuzalisha nafasi za ajira, elimu, ulinzi, kuboresha miundombinu na kuwa na Serikali itakayosaidia kuimarisha umoja wa kitaifa.
“Serikali yangu pia itasimamia sheria ipasavyo ikiwamo kuwasilisha miswada bungeni na kusimamia utekelezaji wa Katiba Mpya ya nchi hiyo.

“Pia suala la usalama ni muhimu sana, tunatakiwa kuongeza idadi ya polisi, kuwajengea uwezo wa vifaa na kuboresha masilahi yao,” alisema Kenyatta.
Katika suala la elimu, Kenyatta alisema wanafunzi wote watakaoanza darasa la kwanza mwaka kesho na wale wanaoingia vyuo vya elimu ya juu watapatiwa kompyuta pakatwa (laptop).
Hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake alizotoa wakati wa kampeni iliyompa ushindi.
Alieleza kwamba vyuo vya elimu ya juu pia vinatakiwa viongezwe kwenye kaunti zote ili kuzuia vyuo vya elimu ya kati kutumika kama vyuo vikuu.
Katika suala la ajira, Uhuru alieleza kwamba upo umuhimu wa kuwawezesha vijana na wanawake kupata ajira, mfuko maalumu umeanzishwa, ambapo fedha za miradi zitatakiwa kupelekwa kwenye ngazi ya majimbo.
Kenyatta alisema kwamba kwa sasa upo umuhimu wa kuangalia zaidi kwenye mapinduzi ya viwanda na kuhakikisha kwamba wanaandaa na kuboresha bidhaa za ndani.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...