Language

Tuesday 19 March 2013

MICHEZO: TIMU TATU ZIMESHUSHWA DARAJA

Release No. 050
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Machi 19, 2013
 
TIMU TATU ZASHUKA DARAJA FDL
Timu tatu zimeshuka daraja kutoka Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kurudi Ligi ya Mkoa msimu ujao wa 2013/2014 baada ya kushika nafasi za mwisho katika ligi hiyo msimu huu 2012/2013 iliyomalizika wikiendi iliyopita.

Small Kids ya Rukwa imeporomoka kutoka kundi A baada ya kuondolewa kwenye michuano hiyo mapema kwa kushindwa kufika uwanjani kwenye moja ya mechi zake. Kwa mujibu wa kanuni matokeo yote ya mechi ilizocheza yalifutwa.
Moro United ya Dar es Salaam ndiyo iliyoaga FDL kutoka kundi B baada ya kumaliza mechi zake ikiwa na pointi tatu. Wakati kutoka kundi C timu iliyoshuka ni Morani ya Manyara iliyomaliza ligi ikiwa na pointi kumi na moja.
Timu zilizopanda daraja kucheza Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2013/2014 ni Mbeya City ya Mbeya iliyoongoza kundi A ikiwa na pointi 31, vinara wa kundi B timu ya Ashanti United ya Dar es Salaam yenye pointi 29 wakati Rhino Rangers ya Tabora imepanda kutoka kundi C ikiwa na pointi 32.

LIUNDA KUTATHIMINI WAAMUZI KOMBE LA DUNIA
Mwamuzi Msaidizi wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Leslie Liunda ameteuliwa kuwa mtathimini wa waamuzi (referee assessor) kwenye moja ya mechi za mchujo za Kombe la Dunia.
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limemteua Liunda kutathimini waamuzi kwenye mechi kati ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Libya itakayochezwa Jumapili (Machi 24 mwaka huu).
Mechi hiyo itafanyika kwenye Uwanja wa Martyrs jijini Kinshasa kuanzia saa 9.30 alasiri kwa saa za Afrika ya Kati (CAT).
Waamuzi watakaochezea mechi hiyo William Selorm Agbovi atakayekuwa mwamuzi wa kati, Malik Alidu Salifu (mwamuzi msaidizi namba moja), David Laryea (mwamuzi msaidizi namba mbili) na mwamuzi wa mezani (fourth official) Cecil Amatey Fleischer. Waamuzi wote hao wanatoka Ghana.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...