Language

Wednesday 27 March 2013

WAKIMBIZI SOMALIA WANADHU


Shirika la kutetea haki za kibinadamu, Human Rights Watch, limesema kuwa makundi yaliyojihami nchini Somalia ikiwemo majeshi ya serikali, yamefanya vitendo vya ubakaji, kuwachapa na kuwadhulumu watu walioachwa bila makao au wakimbizi.

Ripoti ya shirika hilo imegusia wale watu waliokimbia vita tangu mwaka 2011 kwa sababu ya njaa, na sasa wanaishi katika kambi mjini Mogadishu.
Katika ripoti hiyo mpya, shirika hilo limesema kuwa wasimamizi wa kambi hizo , wanaojulikana kama walinzi, huiba msaada wa wakimbizi hao na hata kuwadhulumu.

Shirika hilo linasema , kuwa wakimbizi wa ndani, hasa wanawake wameripoti kubakwa na kudhulumiwa na watu waliovalia sare za kijeshi na wengine wanaoaminiwa kuwa wapiganaji wa makundi ya waasi.
Linasema kuwa baadhi ya vitendo vibaya vya dhuluma walivyofanyiwa ni pamoja na dhulma za kingono dhidi ya wanawake na wasichana.
Kadhalika ripoti hiyo imewanukuu wanawake wanaodai kubakwa akiwemo mwanamke mwenye umri wa miaka
23 aitwaye, Quman.
Anasema alikuwa na ujauzito wa miezi, tisa alipobakwa na kundi la watu asiowajua ingawa walikuwa wamevalia magwanda ya kijeshi.
Mwanamke mwingine, Safiyo, alilazimika kukatwa mguu wake baada ya kubakwa na kisha kupigwa risasi.
Aidha ripoti hiyo inasema kuwa visa vya ubakaji haviripotiwi sana kwa sababu ya hofu ya wanawake kuwa watafanyiwa unyanyapaa na kutengwa na jamii.
''Uchunguzi wetu umeonyesha kuwa watu katika kambi hizo huwekwa kama watumwa. Hawawezi kuondoka, walinzi wa kambi hizo wenyewe wanafanya dhulma. Wao huiba msaada ambao hutolewa kwa wakimbizi. Watu wengi kwa sasa wanahitaji msaada wa haraka,'' ilinukuu ripoti hiyo.
Human Rights Watch pia limefichua visa vya ubaguzi wa kikabila hasaa kwa wale wanaotoka katika jamii fulani. Linasema kuwa watu wengi wamelalamika kuhusu visa vya kukamatwa kiholela na hata kudhulumiwa. Licha ya serikali ya mpya ya Somalia kupiga hatua bado inakabiliwa na changamoto nyingi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...