Language

Saturday 13 April 2013

MBUNGE ALLY KEISSY ATAKA BANGI IHALALISHWE TANZANIA



Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Keissy (CCM), jana aliwavunja mbavu wabunge baada ya kuitaka Serikali kutoa tamko la kuruhusu bangi kuwa zao halali la biashara kwa manufaa ya nchi na wananchi wake.

Keissy ambaye amezoeleka bungeni kama mzee wa kulipua mabomu, alitoa kauli hiyo kupitia swali lake la nyongeza ambapo alisema zao la tumbaku nchini, halina maana kwa sasa zaidi ya bangi.
“Mimi naona hakuna sababu ya kuendelea kusimamia mazao ambayo hata dunia nzima wanayakataa kwa sababu yana ugonjwa wa kansa, leo Serikali itoe tamko ni lini itaruhusu zao la bangi kulimwa kama zao la biashara ili wananchi walime kwa uhuru,” aliuliza Keissy.
Alisema kuna faida kubwa katika kulima bangi kuliko kuendelea kulima zao ambalo watu wengine duniani wameliona kuwa halifai.
Katika swali lake la msingi, Mbunge wa Mpanda Vijijini, Selemani Kakoso (CCM), alitaka kujua ni lini zao la tumbaku litaingizwa kwenye ruzuku ya Serikali ili kupunguza gharama za pembejeo kwa wakulima wa zao hilo.

Mbunge huyo pia alitaka kujua ahadi ya Serikali ya kupunguza ushuru kutoka asilimia tano hadi kufikia asilimia mbili itatekelezwa lini.
Akijibu maswali hayo kwa pamoja, Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Adam Malima alikiri kuwa zao la tumbaku ni zao ambalo linaingiza fedha nyingi za kigeni kuliko mazao mengine ya biashara, lakini halina ruzuku ya pembejeo kama ilivyo kwa mazao mengine.
Malima alisema kutopata ruzuku kwa zao hilo, kunatokana na ufinyu wa bajeti na uwezo wa zao lenyewe kujihami.
Kuhusu bangi, alisema “Tanzania haijaweza kuhalalisha zao la bangi, hivyo tusilinganishe na zao la tumbaku ambalo Tanzania limeonekana kuwa na ubora wa kimasoko hadi China.”

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...